Kocha aliyeitesa Yanga, atua Singida United

Taarifa zinaeleza aliyekuwa Kocha wa Mbao FC, Etienne Ndayiragije amefikia makubaliano na klabu ya Singida United ili kuchukua nafasi ya Mholanzi, Hans van der Pluijm.

Ndayiragije ataanza kuiandaa timu hiyo kwa msimu ujao mara baada ya Pluijm kuondoka rasmi ndani ya kikosi hicho cha walima alizeti mwishoni mwa msimu huu.

Kocha ambaye anakumbukwa kwa kuipa vipigo Yanga tangu ipande daraja, alisajiliwa na Mbao FC akitokea Vital’O ya Burundi.

Mrundi huyo alikuwa akiipa wakati mgumu Yanga ambapo mara ya mwisho wakati timu hizo zilipokutana CCM Kirumba, Mwanza, Yanga ilipoteza kwa mabao 2-0.

Mholanzi Plujim tayari ameshaagana na uongozi wa Singida na inaelezwa kuwa tayari ameshamalizana na Azam FC ili kuchukua nafasi ya Mromania, Aristica Cioba aliyeondoshwa baada ya kushindwa kuonesha kile kilichotarajiwa kwa matajiri hao wa Dar es Salaam.

Leave a comment